Mahakama Kuu ya Guinea imemthibitisha Jenerali Mamadi Doumbouya kuwa mshindi wa uchaguzi wa rais uliofanyika Disemba 28, na hivyo kumfanya rasmi kuwa rais aliyechaguliwa, miaka minne baada ya kuongoza mapinduzi ya kijeshi nchini humo.
Kwa mujibu wa mamlaka ya uchaguzi, Doumbouya alipata asilimia 86.7 ya kura katika uchaguzi wa kwanza tangu mapinduzi ya 2021. Ushindi huo, uliokuwa unatarajiwa na wachambuzi wa siasa, uliridhiwa na Mahakama Kuu katika mji mkuu Conakry.
Akizungumza baada ya kutangazwa kwa matokeo, Doumbouya alisema taifa hilo halina walioshindwa wala walioshinda, akisisitiza umuhimu wa umoja wa kitaifa. Aliwahimiza raia kushirikiana kujenga Guinea yenye amani, haki, ustawi wa pamoja na uhuru wa kisiasa na kiuchumi.
Mpinga wake wa karibu, Yero Baldé, aliyepata asilimia 6.59 ya kura, alikuwa amewasilisha pingamizi dhidi ya matokeo, lakini mamlaka zilisema aliliondoa kabla ya Mahakama Kuu kutoa uamuzi wake.
Uchaguzi huo ulifanyika chini ya katiba mpya iliyoruhusu viongozi wa kijeshi kugombea urais na kuongeza muda wa muhula wa rais kutoka miaka mitano hadi saba. Hata hivyo, wakosoaji wanadai mazingira ya kisiasa hayakuwa huru kikamilifu, wakieleza kuwa upinzani ulikuwa dhaifu kutokana na shinikizo dhidi ya wakosoaji wa serikali.
Licha ya kuwa na utajiri mkubwa wa rasilimali za madini, hususan bauxite, Guinea bado inakabiliwa na changamoto kubwa za kiuchumi, huku zaidi ya nusu ya wananchi wake wakiishi katika umaskini na uhaba wa chakula.
CHANZO: TRT Afrika














