Umoja wa Mataifa umeonya kuwa misaada ya chakula nchini Sudan itakoma kufikia mwishoni mwa Machi iwapo hakutapatikana ufadhili mpya wa haraka. Hali hii inazidisha hofu kwa mamilioni ya watu wanaokabiliwa na moja ya migogoro mikubwa ya njaa duniani.
Kwa sasa, zaidi ya watu milioni 21 – karibu nusu ya idadi ya wananchi – wanakabiliwa na uhaba wa chakula. Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) limesema tayari limepunguza mgao wa chakula wa kuokoa maisha kutokana na ukosefu wa rasilimali.
Onyo hili linakuja baada ya takribani miaka mitatu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe kati ya jeshi na wanamgambo wa RSF, ambavyo vimesababisha vifo vya maelfu na kuwahamisha watu milioni 11 kutoka makazi yao. Umoja wa Mataifa umethibitisha kuwa njaa imeanza kushika kasi katika miji ya El Fasher (Darfur Kaskazini) na Kadugli (Kordofan), maeneo yaliyoathiriwa moja kwa moja na mapigano.
CHANZO: TRT Afrika














