Waziri wa mambo ya nje wa Misri ametoa wito wa kufanyika mabadiliko makubwa katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, akisema muundo wake wa sasa hauakisi uhalisia wa enzi hizi na halitendei haki bara la Afrika, nchi za Kiarabu, na zile za Kiislamu.
Akizungumza katika Jukwaa la Kimkakati la Bled huko Slovenia, Badr Abdelatty amesema kuwa uhusiano wa mataifa mengi hauwezi kufikiwa bila kufanya mabadiliko ya kitaasisi.
“Baraza la Usalama na taasisi za Bretton Woods (Benki ya Dunia na IMF) lazima zifanyiwe mabadiliko. Bila haya, mazungumzo ya uongozi wa dunia na uhusiano wa mataifa hayana maana,” aliliambia jopo kuhusu mchakato huo siku ya Jumanne.
Mjadala kuhusu kura ya turufu
Amesema si sahihi kuwa bara zima la Afrika halijawakilishwa kwa nafasi ya kudumu katika Baraza la Usalama.
“Kuwapa uwezo wa kura ya turufu nchi tano pekee ni suala lililopitwa na wakati na lisilo la kidemokrasia,” Abdelatty alisema, akiongeza kuwa haki hiyo iongezwe kwa wanachama wapya au iondolewe moja kwa moja.
Abdelatty alishtumu serikali za magharibi kwa undumakuwili, akieleza tofauti ya namna masuala ya uvamizi wa Ukraine na Urusi na vita vya Israel huko Gaza yalivyoshughulikiwa.














