Benki Kuu ya Uganda imeeleza wasiwasi mkubwa kuhusu mswada mpya unaolenga kudhibiti ushawishi wa fedha za kigeni katika siasa, ikionya kuwa unaweza kuathiri vibaya uchumi wa nchi.
Mswada huo unaoitwa The Protection of Sovereignty Bill, 2026 unapendekeza kuwa mtu yeyote anayepokea ufadhili wa kigeni unaozidi dola 106,300 ndani ya miezi 12 lazima apate kibali cha maandishi kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Ndani.
Gavana wa Benki Kuu, Michael Atingi-Ego, amesema utekelezaji wa sheria hiyo unaweza kupunguza mtiririko wa fedha kutoka nje, jambo litakaloathiri akiba ya taifa ya fedha za kigeni.
Kwa sasa Uganda ina karibu dola bilioni 6 za akiba ya fedha za kigeni, ambazo Benki Kuu inasema ziko hatarini iwapo mswada huo utapitishwa.














