Mabalozi wawili wa Marekani wamethibitisha hadharani kuwa Israel ilipeleka mfumo wake wa ulinzi wa Iron Dome na wanajeshi katika Falme za Kiarabu wakati wa vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran, hii ikiwa ni taarifa ya kwanza rasmi kukiri matumizi ya mfumo huo katika taifa la Ghuba.
Balozi wa Marekani nchini Israel Mike Huckabee amethibitisha hayo katika hafla moja mjini Tel Aviv siku ya Jumanne, akisema Israel ilituma mfumo wa Iron Dome na wanajeshi kusaidia kulinda UAE wakati wa mapigano.
“Ningependa kutoa shukrani kwa nchi mwanachama ya kwanza ya makubaliano ya Abraham,” Huckabee alisema katika kongamano mjini Tel Aviv. “Tizama faida. Israel inawapelekea mfumo wa ulinzi wa Iron Dome na wanajeshi wa kuwasaidia katika kuutumia.”
Matamshi ya Huckabee yanakuja siku moja baada ya Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Mike Waltz kuthibitisha kuwa mfumo wa ulinzi wa Israel wa Iron Dome ulitumika kuzuia makombora ya Iran yaliyokuwa yanashambulia UAE, ikiwa ni thibitisho la kwanza rasmi hadharani kuwa mfumo huo ulipelekewa na kutumika katika taifa hilo la Ghuba wakati wa vita vya hivi karibuni.
UAE, taifa la muungano wa mamlaka saba katika Rasi ya Arabuni, iliitambua Israel rasmi kidiplomasia 2020.
UAE haikujibu ombi la kutaka wazungumzie kukiri kwa Huckabee, ingawa hili lilidhihirisha kuimarika kwa uhusiano katika masuala ya kijeshi ya mataifa hayo mawili ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakiitilia shaka Iran.














