Mke wa Rais wa Marekani, Donald Trump, Melania Trump anatarajiwa kuongoza kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kitakachofanyika Jumatatu, Machi 2, 2026. Kwa mujibu wa taarifa kutoka ofisi yake, hatua hiyo itamfanya kuwa mke wa kwanza wa rais aliye madarakani kuongoza kikao hicho muhimu katika historia ya Umoja wa Mataifa.
Tukio hilo linajiri wakati kukiwa na mvutano mkubwa wa kisiasa na kijeshi, kufuatia mashambulizi ya hivi karibuni ya Marekani na Israel dhidi ya Iran.
Melania Trump, ambaye awali alikuwa mwanamitindo, amewahi kushiriki katika masuala ya kidiplomasia, ikiwemo juhudi za kuachiliwa huru kwa watoto wa Ukraine waliokuwa wakishikiliwa nchini Urusi.
Katika miaka ya karibuni, kumekuwepo mvutano kati ya Marekani na Umoja wa Mataifa, huku baadhi ya wachambuzi wakidai kuwa Rais Trump anajaribu kupanua ushawishi wake ndani ya taasisi hiyo kupitia kile kinachoitwa “Bodi ya Amani” iliyoanzishwa mwezi uliopita.
CHANZO: TRT Afrika














