Ajenda Afrika

Helikopta ya Uokoaji Yaanguka Mlima Kilimanjaro

“Ajali hii imetokea wakati helikopta ikiwa kwenye misheni ya kuokoa maisha ya binadamu, tukio linalosikitisha sana,” alisema Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa.

Newstimehub

Newstimehub

25 Desemba, 2025

200

Helikopta iliyokuwa ikitekeleza operesheni ya uokoaji kwenye Mlima Kilimanjaro nchini Tanzania imeanguka na kuua watu wote waliokuwemo ndani yake. Tukio hilo lilitokea Jumatano jioni kwenye moja ya njia zinazotumiwa sana na watalii wanaopanda mlima huo.

Kwa mujibu wa polisi, helikopta hiyo ilikuwa kwenye misheni ya dharura ya kuwachukua wagonjwa waliokuwa kwenye mlima huo. Miongoni mwa waliopoteza maisha ni raia wawili wa kigeni waliokuwa wamehamishwa kwa matibabu, pamoja na daktari wa eneo hilo, mwongoza watalii na rubani wa helikopta hiyo.

Ajali hiyo ilitokea kati ya Kambi ya Barafu na Kilele cha Kibo, katika eneo lenye mwinuko wa zaidi ya mita 4,000 juu ya usawa wa bahari. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa, alisema helikopta hiyo ilikuwa mali ya kampuni ya Kilimanjaro Aviation, ambayo hutoa huduma za uokoaji na usafiri wa anga wa dharura.

Hadi sasa, kampuni husika haijatoa tamko rasmi kuhusu tukio hilo. Polisi wamesema taarifa zaidi zitatolewa baadaye, huku uchunguzi ukiendelea kubaini chanzo cha ajali hiyo.

Ajali za ndege katika Mlima Kilimanjaro ni nadra kutokea, na tukio la mwisho liliripotiwa mwaka 2008, ambapo watu wanne walipoteza maisha.

CHANZO: TRT Afrika