Ulimwengu

Trump: Marekani itachagua kampuni za mafuta zitakazoruhusiwa kufanya kazi Venezuela

Marekani itaamua nani anafanya kazi Venezuela, kwa maslahi ya usalama na uchumi wake.

Newstimehub

Newstimehub

10 Januari, 2026

251

Rais wa Marekani Donald Trump amesema serikali yake iko karibu kutoa uamuzi kuhusu ni kampuni zipi za mafuta zitapewa ruhusa ya kufanya kazi nchini Venezuela. Akizungumza Ikulu ya White House wakati wa mkutano na wakurugenzi wa kampuni kubwa za mafuta, Trump alisema uamuzi huo unaweza kutolewa hivi karibuni, akisisitiza kuwa kampuni zitawasiliana moja kwa moja na Washington, si serikali ya Caracas.

Trump aliwaambia viongozi wa kampuni hizo kuwa Marekani haitaki biashara ya moja kwa moja na Venezuela, lakini akawahakikishia kile alichokiita “usalama wa jumla” endapo watatii masharti ya Marekani. Maafisa wa utawala wake wamesema lengo ni kudhibiti mauzo na mapato ya mafuta ya Venezuela ili yaendane na maslahi ya Marekani, huku wakihimiza uwekezaji wa mabilioni ya dola katika ukarabati wa miundombinu ya mafuta ya nchi hiyo.

Makampuni makubwa kama Chevron, ExxonMobil na ConocoPhillips, pamoja na wafanyabiashara wa mafuta kama Vitol na Trafigura, yanatajwa kuwania vibali vya kuuza mafuta ghafi ya Venezuela. Hata hivyo, makampuni mengi yana wasiwasi kuwekeza kwa muda mrefu kutokana na hali ya kisiasa isiyotabirika na gharama kubwa za uendeshaji.

Wakati huo huo, Venezuela imethibitisha kuwa iko katika mazungumzo ya awali na Marekani kuhusu kurejesha uhusiano wa kidiplomasia uliokatika mwaka 2019. Serikali ya Caracas imesema itajibu hatua ya Washington, baada ya wanadiplomasia wa Marekani kusafiri kuelekea mji mkuu huo kwa majadiliano yanayohusiana na kufungua tena ubalozi wa Marekani.

CHANZO: TRT Afrika