Afrika Ulimwengu

Maseneta wa Marekani waonya kuhusu hali ya kibinadamu mashariki mwa DRC

Maseneta wa Marekani wameonesha wasiwasi kuhusu sehemu za mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kuendelea kukaliwa na kundi la waasi wa M23.

Newstimehub

Newstimehub

5 Februari, 2026

401

Maseneta wa Marekani wameeleza wasiwasi mkubwa kuhusu kuendelea kwa kundi la waasi wa M23 kudhibiti maeneo ya mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). Katika mkutano wao na Rais Felix Tshisekedi, walibainisha kuwa mgogoro wa kibinadamu unaoendelea umesababisha zaidi ya watu milioni 26 kukabiliwa na uhaba wa chakula, hali waliyotaja kuwa isiyovumilika.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa na mataifa ya Magharibi, M23 inaungwa mkono na Rwanda, ingawa Kigali imekuwa ikikanusha tuhuma hizo. Kundi hilo linadhibiti miji muhimu ya Goma na Bukavu tangu mapema 2025, na hivi karibuni muungano wa kisiasa wa Congo River Alliance – unaojumuisha wapiganaji wa M23 – ulikiri kuhusika na shambulio katika Uwanja wa Ndege wa Bangoka, Kisangani.

Mkutano wa Jumatano ulijadili pia Makubaliano ya Washington ya Amani na Maendeleo, pamoja na mustakbali wa ushirikiano kati ya Marekani na DRC. Kamati ya Mambo ya Nje ya Seneti imesisitiza kuwa Rwanda inapaswa kujiondoa kikamilifu katika eneo la mashariki ili kutoa nafasi ya amani ya kudumu. Aidha, Washington imeeleza utayari wa kuimarisha ushirikiano na DRC, huku ikiahidi kuchukua hatua dhidi ya wale wanaovunja makubaliano ya amani yaliyosainiwa Disemba 2025 kati ya Tshisekedi na Paul Kagame.

CHANZO: TRT Afrika