Ushiriki wa Uganda katika Kongamano la Diplomasia la Antalya nchini Uturuki umeonyesha wazi dhamira ya taifa hilo la Afrika Mashariki kuendelea na mazungumzo ya kidiplomasia na ushirikiano wa kimataifa.
Hatua hiyo imekuja licha ya mvutano uliosababishwa na matamshi ya mkuu wa jeshi la Uganda, Muhoozi Keinerugaba, aliyewahi kutishia kukata uhusiano wa kidiplomasia na Ankara kutokana na ushawishi wa Uturuki nchini Somalia.
Hata hivyo, Kampala imeonyesha ishara ya kuheshimu mazungumzo kwa kushiriki katika jukwaa hilo, hatua inayotafsiriwa kama nia ya kuimarisha uhusiano wa muda mrefu kati ya nchi hizo mbili ambao umeendelea kwa zaidi ya miaka 50.
Ushirikiano huo umeonekana katika sekta mbalimbali zikiwemo elimu, ulinzi na uchumi. Mamia ya wanafunzi wa Uganda wamefaidika na ufadhili wa masomo kupitia mpango wa Turkiye Burslari, huku vyuo vikuu vya nchi hizo vikishirikiana kitaaluma.
Aidha, ushirikiano wa kiulinzi umeimarishwa tangu ziara ya Rais Recep Tayyip Erdogan nchini Uganda mwaka 2016, ambapo mikataba muhimu ilisainiwa.
CHANZO: TRT Afrika














