Libya imefikia kiwango cha juu cha uzalishaji wa mafuta tangu mwaka 2013, ikizalisha mapipa milioni 1.37 kwa siku mwaka 2025. Waziri Mkuu Abdulhamid Dbeibah alisema uzalishaji huo uliongezeka baada ya kufunguliwa tena mashamba kadhaa ya mafuta nchini.
Akizungumza katika mkutano wa Libya Energy and Economy Summit 2026 mjini Tripoli, Dbeibah alieleza kuwa Libya ilizindua mnamo 2025 zabuni ya kwanza ya leseni za utafiti wa mafuta na gesi baada ya miaka 17, jambo lililovutia mashirika makubwa ya kimataifa. Matokeo ya zabuni hiyo yanatarajiwa kutangazwa Februari.
Aidha, mikataba mipya inatarajiwa kusainiwa ili kuendeleza visima viwili vya gesi baharini. Libya, mwanachama wa OPEC, inakadiriwa kuwa na akiba ya mapipa ya mafuta bilioni 48.4 na gesi asilia takriban trilioni 1.5 za mita za ujazo.
Kwa kuwa na jua la kutosha na ardhi kubwa, Libya pia ina uwezo mkubwa wa kuendeleza nishati mbadala. Kipaumbele cha taifa kimekuwa ni kudumisha uzalishaji wa mafuta na gesi, kuboresha miundombinu ya nishati na kuunganisha vyanzo vya nishati safi katika mfumo wa kitaifa.
CHANZO: TRT Afrika














