Serikali ya Zanzibar imetangaza mpango wa kuanza kununua mchanga kutoka Tanzania Bara ili kusaidia utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo inayofanyika visiwani humo.
Akizungumza na waandishi wa habari, Waziri wa Maji, Nishati na Madini wa Zanzibar Nadir Abdul Latif alisema hatua hiyo imechukuliwa baada ya serikali kubaini kuwa mahitaji ya mchanga kwa miradi mikubwa ya ujenzi yameongezeka kwa kiasi kikubwa.
Alisema mchanga huo utatumika hasa katika miradi mikubwa ya ujenzi inayotekelezwa na serikali pamoja na ile inayohusisha uwekezaji mkubwa ili kuhakikisha miradi hiyo inaendelea bila kukwama kutokana na upungufu wa mchanga.
Waziri huyo alieleza kuwa mpango huo pia unalenga kupunguza uchimbaji mkubwa wa mchanga ndani ya Zanzibar ambao unaweza kusababisha madhara kwa mazingira kama vile mmomonyoko wa udongo na uharibifu wa ardhi.
CHANZO: TRT Afrika














