Afrika

Guinea-Bissau: Serikali ya kijeshi yabadilisha katiba, yakipa rais mamlaka makubwa

CNT limepitisha kwa kauli moja marekebisho ya katiba, yakibadilisha mfumo wa utawala kuwa wa urais.

Newstimehub

Newstimehub

15 Januari, 2026

280

Mwezi mmoja na nusu baada ya mapinduzi ya kijeshi yaliyoongozwa na Jenerali Horta N’Tam, Baraza la Kitaifa la Mpito (CNT) nchini Guinea-Bissau limepitisha kwa kauli moja marekebisho ya katiba. Hatua hii inakuja baada ya jeshi kumwondoa madarakani Rais Umaro Sissoco Embaló mnamo Novemba 26, muda mfupi baada ya uchaguzi wa urais, na kusimamisha mchakato wa uchaguzi kwa mwaka mmoja.

Marekebisho hayo yanabadilisha mfumo wa utawala kutoka bunge lenye nguvu kwenda mfumo wa urais. Katika katiba mpya, rais atakuwa na mamlaka ya kuteua waziri mkuu na mawaziri, pamoja na uwezo wa kulivunja bunge. Aidha, jina la Bunge la Kitaifa la Watu limebadilishwa na sasa litaitwa Bunge la Kitaifa.

Awali, waziri mkuu alitokana na chama chenye wingi bungeni, hali iliyosababisha migongano ya kisiasa, ikiwemo kuvunjwa kwa bunge na Rais Embaló mnamo Desemba 2023. Kabla ya kuondolewa kwake, Embaló alikuwa akiongoza kwa amri za urais.

Guinea-Bissau imekuwa ikikumbwa na misukosuko ya kisiasa kwa muda mrefu, ikiwa na historia ya mapinduzi manne ya kijeshi na majaribio kadhaa ya uasi tangu kupata uhuru kutoka Ureno mwaka 1974.

CHANZO: TRT Afrika