Afrika Ajenda

Mabilionea wa Afrika waongoza kwa kasi ya ukuaji wa utajiri 2026

Dangote ameongeza utajiri wake kwa $451m na kufikia $30.4b.

Newstimehub

Newstimehub

15 Januari, 2026

286

Ripoti mpya ya Bloomberg inaonyesha kuwa mabilionea wa Nigeria, Aliko Dangote na Abdul Samad Rabiu, ndio wanaoongoza kwa kasi ya ukuaji wa utajiri barani Afrika mwaka 2026. Dangote, tajiri mkubwa zaidi barani, ameongeza utajiri wake kwa dola milioni 451 katika wiki mbili za kwanza za mwaka, na kufikia jumla ya dola bilioni 30.4, akishika nafasi ya 79 duniani.

Rabiu, mwenye umri wa miaka 65, pia ameongeza utajiri wake kwa dola milioni 328 na kufikia jumla ya dola bilioni 10.8, akishika nafasi ya nne barani na ya 337 duniani. Wote wawili wanatoka mjini Kano, kaskazini mwa Nigeria.

Dangote amepanua biashara zake kupitia Dangote Group katika sekta za mafuta, mbolea, saruji na chakula, huku Rabiu akiongoza BUA Group inayoshughulika na chakula, saruji, mali isiyohamishika, miundombinu na madini.

Mabilionea wengine waliopata ongezeko la utajiri mwaka huu ni Johann Rupert wa Afrika Kusini (+$70.9m, jumla $19.5b), Naguib Sawiris wa Misri (+$173m, jumla $10.8b), na Natie Kirsh wa Afrika Kusini (+$289m, jumla $10b).

Hata hivyo, ripoti za kimataifa zinaonya kuwa ukuaji huu wa utajiri unakuja sambamba na kuongezeka kwa pengo la usawa wa mapato duniani. Ripoti ya World Inequality ya 2025 ilibainisha kuwa asilimia 10 ya watu duniani wanamiliki asilimia 75 ya utajiri wote, huku kusini mwa Afrika pengo hilo likihusishwa na urithi wa utawala wa ubaguzi wa rangi.

CHANZO: TRT Afrika