Morocco imefungua rasmi mnara wake mpya wa kisasa wa Mohammed VI Tower, jengo la kifahari lenye thamani ya dola milioni 700, katika mji wa Salé karibu na mji mkuu Rabat.
Mnara huo wenye ghorofa 55 na urefu wa futi 820 umepewa jina la Mfalme Mohammed VI na umeundwa kwa mtindo unaofanana na roketi inayozinduliwa.
Ndani ya jengo hilo kutakuwa na hoteli ya kifahari ya Waldorf Astoria, ofisi, maduka, migahawa na makazi ya hali ya juu.
Maafisa wa maendeleo wanasema mradi huo unatarajiwa kuzalisha ajira 450 za moja kwa moja na zaidi ya ajira 3,500 zisizo za moja kwa moja.
Ujenzi wa jengo hilo ulidumu kwa miaka minane na ulihusisha zaidi ya wafanyakazi 2,500 kutoka zaidi ya nchi 12.
Morocco imesema mradi huo unaonyesha dhamira yake ya kujiweka kama nguvu kubwa ya kikanda kupitia miradi mikubwa ya maendeleo.














