Afrika Ulimwengu

Uingereza yaweka masharti magumu ya viza kwa raia wa DRC kutokana na changamoto za urejeshaji wahamiaji

Uingereza imeamua kuweka vizuizi vya viza kwa raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kutokana na ushirikiano mdogo katika kurejesha wahamiaji haramu.

Newstimehub

Newstimehub

29 Desemba, 2025

211

Serikali ya Uingereza imetangaza kuanzisha vizuizi vipya vya utoaji viza kwa raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), ikieleza kuwa hatua hiyo imesababishwa na ukosefu wa ushirikiano wa nchi hiyo katika kuwapokea wahamiaji wasiokuwa na nyaraka halali wanaorejeshwa kutoka Uingereza.

Kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Uingereza, hatua kali zaidi, ikiwemo kusitishwa kabisa kwa utoaji wa viza, zinaweza kuchukuliwa endapo DRC haitaboresha ushirikiano wake kwa haraka.

Vikwazo hivyo vinawaathiri hasa maafisa waandamizi na watunga sera wa DRC, ambao hawatapata tena huduma maalum za viza. Aidha, mfumo wa kutoa viza kwa haraka umeondolewa kwa raia wote wa taifa hilo.

Hatua hiyo inafuatia onyo lililotolewa mwezi Novemba na Waziri wa Mambo ya Ndani wa Uingereza, Shabana Mahmood, kwa mataifa ya DRC, Angola na Namibia, akisema yangewekewa marufuku ya viza iwapo yasingekubali kuwapokea raia wao waliokuwa wakirejeshwa.

Wizara ya mambo ya ndani ilieleza kuwa nchi hizo tatu zimekuwa zikikwamisha mara kwa mara juhudi za kuwarejesha wahamiaji haramu, kwa kukataa kuwapokea raia wao au kuweka masharti ya kisheria yanayochelewesha mchakato huo.

Hata hivyo, Angola na Namibia zilikubali kuboresha taratibu zao za urejeshaji na kuanza kuwapokea wahamiaji waliorejeshwa, hatua iliyozifanya kuepuka vikwazo vya viza.

Kwa upande wa DRC, wizara ilibainisha kuwa mazungumzo bado yanaendelea, lakini ikaonya kuwa nchi hiyo inapaswa kuzingatia wajibu wake wa kisheria wa kuwapokea raia wake.

Hatua hizi za viza ni sehemu ya mpango mpana wa Uingereza wa kuimarisha sheria za uhamiaji na kuifanya mifumo ya kuomba hifadhi kuwa mikali zaidi, mpango uliotangazwa mwezi Novemba.

CHANZO: TRT Afrika