Afrika

Wakazi wa Mogadishu wapiga kura kuchagua viongozi wa mitaa

Kupiga kura moja kwa moja kunarejesha sauti ya raia katika uamuzi wa uongozi wa maeneo yao.

Newstimehub

Newstimehub

25 Desemba, 2025

202

Raia wa mji wa Mogadishu, ambao ni makao makuu ya Somalia, wameanza kushiriki zoezi la kupiga kura siku ya Alhamisi ili kuwachagua viongozi wa ngazi za mitaa, hatua ambayo haijawahi kushuhudiwa kwa njia ya kura ya moja kwa moja tangu mwaka 1969.

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi na Mipaka ya Somalia ilithibitisha kuwa vituo vya kupigia kura vilifunguliwa mapema, huku wananchi wakianza kushiriki zoezi hilo linalolenga kuunda uongozi wa maeneo mbalimbali ya kiutawala.

Kwa mujibu wa taarifa ya tume hiyo, jumla ya wagombea 1,604 kutoka vyama vya siasa 20 wanawania nafasi mbalimbali katika uchaguzi huo, ambao unatarajiwa kukamilika jioni ya siku hiyo hiyo.

Viongozi wa serikali wamesema kufanikiwa kwa zoezi hilo katika mji mkuu kutafungua njia ya kuanzisha uchaguzi wa aina hiyo katika maeneo mengine ya nchi, na hatimaye kuandaa uchaguzi wa kitaifa unaohusisha kura ya moja kwa moja ya wananchi.

Uchaguzi huo umeelezwa kama hatua muhimu katika mabadiliko ya mfumo wa uongozi, kutoka utaratibu wa zamani uliotegemea uwakilishi wa koo, kwenda mfumo unaompa kila raia haki sawa ya kupiga kura.

Tangu kuzuka kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe mwaka 1991, Somalia imekuwa ikitumia mfumo wa kisiasa ambapo wananchi hawakushiriki moja kwa moja katika uchaguzi, huku wabunge wakiteuliwa na wazee wa koo na rais kuchaguliwa na Bunge.

Kwa sasa, serikali ya shirikisho inaendelea na mageuzi ya kisiasa yanayolenga kuimarisha ushiriki wa wananchi katika maamuzi ya uongozi kupitia uchaguzi wa wazi na wa moja kwa moja.

CHANZO: TRT Afrika