Rais wa Kenya, William Ruto, ametangaza kuwa nchi hiyo haitauza tena madini ghafi nje ya nchi, hatua inayolenga kubadilisha mfumo wa uchumi na kuongeza thamani ya rasilimali zake.
Akizungumza katika kongamano la Afrika We Build jijini Nairobi, Ruto alisema kuwa mfumo wa kuuza malighafi bila kuchakatwa umeinyima Kenya manufaa muhimu kama ajira, teknolojia na mapato makubwa.
Alisisitiza kuwa serikali sasa itawekeza katika viwanda vya ndani ili kuhakikisha madini kama titanium, dhahabu na mengine yanachakatwa kabla ya kusafirishwa.
Ruto alitoa mfano wa kampuni ya Base Titanium, akisema Kenya haikupata faida ya kutosha licha ya uwepo wa rasilimali hiyo nchini.
Hatua hiyo inaashiria mabadiliko makubwa ya sera ya rasilimali nchini Kenya.














