Kampuni ya Airtel Africa inapanga kufanya mauzo ya hisa kwa umma (IPO) ya kitengo chake cha huduma za kifedha kinachojulikana kama Airtel Money, katika jiji la London.
Kwa mujibu wa taarifa za karibu na mpango huo, IPO hiyo inaweza kukusanya kati ya dola bilioni 1.5 hadi 2, hatua ambayo inaweza kuiweka kampuni hiyo katika nafasi kubwa zaidi katika soko la fedha barani Ulaya.
Inaelezwa kuwa thamani ya Airtel Money inaweza kufikia hadi dola bilioni 10, kutokana na ukuaji wake mkubwa katika sekta ya fedha kidijitali barani Afrika. Huduma hiyo imekuwa muhimu kwa mamilioni ya watu wasiokuwa na akaunti za benki, kwa kuwawezesha kufanya miamala kwa njia ya simu.
Kampuni hiyo inashirikiana na benki ya uwekezaji ya Citigroup katika maandalizi ya IPO hiyo, huku benki nyingine zikitarajiwa kujiunga katika mchakato huo.
Wataalamu wa uchumi wanaona kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Airtel kupanua huduma zake za kifedha na kuvutia wawekezaji wa kimataifa. Hata hivyo, bado hakuna uamuzi wa mwisho kuhusu muda kamili wa IPO hiyo au maelezo yote ya utekelezaji wake.
Chanzo:The Economic Times














