Ripoti mpya ya Chuo Kikuu cha Boston imeonyesha kuwa mikopo ya China kwa Afrika ilipungua kwa nusu hadi dola bilioni 2.1 mwaka 2024, kiwango cha chini zaidi tangu janga la COVID-19. Hii ni chini ya sehemu ya kumi ya kilele cha dola bilioni 28.8 kilichorekodiwa mwaka 2016.
Mwelekeo huu unaonyesha kuwa Beijing inajiondoa kwenye miradi mikubwa ya miundombinu kama reli na barabara, na badala yake inalenga miradi midogo yenye faida kibiashara. China sasa inatumia zaidi mikopo inayotolewa kwa sarafu ya yuan (RMB), ufadhili kupitia benki za ndani za Afrika kwa biashara ndogo na za kati (SMEs), pamoja na uwekezaji wa moja kwa moja (FDI).
Nchi kama Kenya tayari zimebadilisha mikopo ya thamani ya dola bilioni 3.5 kuwa yuan, huku Ethiopia ikifikiria kufanya hivyo. Angola imekuwa mnufaika mkubwa kwa kupata dola bilioni 1.45 kwa ajili ya kuboresha gridi ya umeme na barabara. Jumla ya miradi sita pekee ilifadhiliwa na China mwaka 2024, ikiwemo Angola, Kenya, Misri, DRC na Senegal.
CHANZO: TRT Afrika














