Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) imetangaza kuanzishwa kwa kikosi maalum cha “walinzi wa migodi” kitakachokuwa na jukumu la kulinda sekta ya madini nchini humo.
Kwa mujibu wa Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Migodi, kikosi hicho kitahakikisha usalama wa maeneo ya uchimbaji, usafirishaji wa madini, pamoja na vituo vya uchakataji na mipaka ya nchi.
Serikali imetenga takribani dola milioni 100 za Marekani kwa ajili ya mafunzo ya miezi sita na ununuzi wa vifaa maalum kwa walinzi hao.
Kundi la kwanza la maafisa kati ya 2,500 hadi 3,000 linatarajiwa kupelekwa katika majimbo 22 ya nchi baada ya mafunzo yatakayoanza Juni hadi Disemba mwaka huu.
Mpango huo ni sehemu ya jitihada za serikali kuimarisha udhibiti wa sekta ya madini ambayo ni uti wa mgongo wa uchumi wa taifa.
CHANZO: TRT Afrika














