Utawala wa kijeshi wa Niger umetangaza kufuta maandamano ya jadi ya Mei Mosi kote nchini kwa sababu za kiusalama, hatua ambayo haijawahi kuchukuliwa awali kwa sababu hiyo.
Katika taarifa iliyotolewa na Wizara ya Kazi ya Niger, serikali imesema maadhimisho ya mwaka huu yatafanyika kwa njia ya ishara badala ya mikusanyiko mikubwa ya hadhara, ili kuepuka hatari za kiusalama.
Niger imekuwa ikikabiliwa na mashambulizi ya mara kwa mara kutoka kwa makundi ya kigaidi katika maeneo ya magharibi na kusini mashariki mwa nchi, hali ambayo imeifanya serikali kuongeza tahadhari.
Waziri wa Kazi Aïssatou Abdoulaye Tondi amesema uamuzi huo umetokana na mazingira ya sasa ya kitaifa yanayokabiliwa na changamoto nyingi hasa za usalama.














