Ajenda Afrika

Marekani na Nigeria zasaini mkataba wa afya wenye msisitizo wa huduma za Kikristo

Marekani na Nigeria zimesaini makubaliano ya miaka mitano ya kuimarisha sekta ya afya, huku Washington ikiahidi kuchangia takriban dola bilioni 2.1.

Newstimehub

Newstimehub

21 Desemba, 2025

169

Marekani imetangaza kusaini makubaliano mapya ya miaka mitano na Nigeria yanayolenga kuimarisha mfumo wa afya wa nchi hiyo, huku yakijumuisha msisitizo maalum kwa huduma za afya zinazotolewa na taasisi za Kikristo. Taarifa hiyo ilitolewa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani Jumamosi.

Kwa mujibu wa makubaliano hayo ya pande mbili, Washington itatoa takriban dola bilioni 2.1 kusaidia juhudi za kuzuia na kudhibiti magonjwa kama VVU, kifua kikuu, malaria na polio, pamoja na kuboresha afya ya mama na mtoto. Nigeria, kwa upande wake, imeahidi kuongeza bajeti yake ya kitaifa ya afya kwa karibu dola bilioni 3 katika kipindi cha miaka mitano ijayo.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani alisema mkataba huo unaweka mkazo mkubwa katika kuendeleza watoa huduma za afya wa msingi wanaofanya kazi kupitia taasisi za imani ya Kikristo. Hatua hiyo inakuja katika muktadha wa matamshi ya hivi karibuni ya Rais wa Marekani, Donald Trump, ambaye alidai kuwa Wakristo nchini Nigeria wanakabiliwa na vitisho vikubwa, madai ambayo yamekanushwa na mamlaka za Nigeria pamoja na watafiti huru.

Mwezi uliopita, Trump alizua mjadala mkali baada ya kusema kupitia mitandao ya kijamii kwamba Marekani iko tayari kuchukua hatua za kijeshi kukabiliana na kile alichokiita “mauaji ya Wakristo” nchini Nigeria. Serikali ya Nigeria imesema changamoto za usalama nchini humo zinaathiri watu wa dini zote, si Wakristo pekee.

Washington pia imeirejesha Nigeria kwenye orodha ya nchi zinazochukuliwa kuwa na “wasiwasi maalum” kuhusu uhuru wa dini, na wakati huo huo imepunguza utoaji wa viza kwa raia wa Nigeria. Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilieleza kuwa makubaliano ya afya yalihusishwa na kile ilichokitaja kama marekebisho yaliyofanywa na serikali ya Nigeria ili kuweka kipaumbele katika kulinda jamii za Wakristo dhidi ya ghasia.

Nigeria ina mgawanyo wa kidini unaokaribia kuwa sawa, ambapo Wakristo wanapatikana zaidi kusini na Waislamu wengi wakiwa kaskazini. Serikali ya Abuja imesisitiza kuwa haitavumilia aina yoyote ya mateso ya kidini.

Tangu mwaka 2009, Nigeria imekuwa ikipambana na makundi ya waasi na magaidi, mgogoro uliosababisha vifo vya zaidi ya watu 40,000 na kuwafanya zaidi ya milioni mbili kuyahama makazi yao, kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa. Makubaliano hayo na Nigeria yanafuatia mkataba mwingine wa afya wa dola bilioni 2.5 uliosainiwa mapema Desemba kati ya Marekani na Kenya, katika kipindi ambacho utawala wa Trump umefanya mabadiliko makubwa katika sera ya misaada ya kigeni kwa kaulimbiu ya “America First.”

CHANZO: TRT Afrika